MAHOJIANO NA GAZETI LA MWANANCHI YALIYOCHAPWA LEO. BAADHI YA - TopicsExpress



          

MAHOJIANO NA GAZETI LA MWANANCHI YALIYOCHAPWA LEO. BAADHI YA MISTARI IMEHA,RIRIWA. Q1. Umepokeaje uamuzi wa serikali kurekebisha viwango vya ufaulu? Jibu: Watu wa umri wangu watakumbuka kwamba wakati tunasoma shule za msingi mitihani yetu na majibu yake vyote vilikuwa siri. Waliofaulu wahakujua wamepata alama gani wala walioshindwa hawakujua wameshindwa nini na kwa kiasi gani. Neno kufaulu halikuwepo katika msamiati wa enzi zetu. Badala yake msamiati wa KUCHAGULIWA ukatawala. Walioenda sekondari walisemekana kwamba wamechaguliwa na wasioenda hawakuchaguliwa. Utaratibu huu uliwezesha wanafunzi wenye uwezo duni kuchaguliwa na waliokuwa na uwezo mkubwa kuachwa. Lakini zaidi uliwanyima fursa walioona wameonewa kulalamika kwa sababu haikusemwa kwamba wamefeli bali walijulishwa kwamba hawakuchaguliwa. Watumishi wasiokuwa waadilifu walitumia mwanya huo kufanya upendeleo ama wa kidini au kikabila. Tatizo hili leo ni historia kwa sababu leo wasiokwenda sekondari na wale wanaoenda kila mmoja anapata fursa ya kujua majibu yake na ukweli ni kwamba wanaosonga mbele inakuwa ni kwa kufaulu siyo kuchaguliwa. Hivyo uamuzi huu kwangu unakwenda sambamba na enzi yetu hii ya uhuru wa habari . Kwamba kwa mara ya kwanza wateja wa NECTA wamepewa haki ya kujua ni kwa namna gani mtu atapata alama katika mitihani ya Taifa. Mzazi, wanafunzi, mwalimu, mkaguzi na viongozi wa elimu sasa wanapata fursa kwa mara ya kwanza katika histori ya Tanzania kujua ni kwa vipi alama ya mwanafunzi itapatikana. Kwangu mimi huu ni uamuzi wa kijasiri ambao hautapendwa na watu wachache ambao kwa muda mrefu wamekuwa na nguvu isiyokuwa na kifani ya kuamua kila mwaka na kwa kila somo ufaulu uwe namna gani huku wateja wote wakiwa gizani. Q2. Unadhani suala la viwango hivyo limewahi kuwa tatizo la msingi katika sekta ya elimu nchini? Swali hili ni subjective kwa vile ni wazi kwamba hakuna tafisri ya kukubalika na wote kuhusu maana halisi ya “tatizo la msingi” wala vigezo vinavyohalalisha tatizo kuwa ni la msingi. Kwa wanaume malalamiko ya wanawake kuhusu mfumo dume huenda hayawakilishi tatizo la msingi juu ya hali ya maisha ya watanzania. Lakini kwa wanawake mfumo dume ni tatizo la msingi la kupewa kipaumbele kutatuliwa ili kuwepo usawa wa fursa katika maendeleo. Watoto wa watu ambao tangu awali wamekuwa wakipata fursa za elimu kuanzi babu , baba, watoto na sasa wajukuu, alama za ufaulu zinazozungumzia 0-50% haliwezi kuwa ni sehemu ya matatizo ya msingi kwao. Hawa ni watu wanaoshughulishwa na ubora kwa maana halisi ya ubora wa elimu. Kwa kuwa sielewi vigezo vya wengine ili jambo liwe tatizo la msingi, mimi nasema kwamba suala hili limekuwa ni tatizo kubwa hasa kwa nchi ambayo rushwa na ufisadi upo kwa kiwango cha juu sana. Utaratibu huu uliotangazwa umeweka bayana mambo yafuatayo: Alama za ufaulu sasa ni mgando (zitafanana kwa masomo yote na hazitabadilika mwaka hadi mwaka), wateja wa NECTA wamejulishwa kwamba mtihani wa mwisho ni alama 60 na mazoezi endelevu ni alama 40, kila alama anayopata mtoto inaumuhimu katika maisha yake ya kielimu na inatambuliwa. Viwango hivi vinamaliza uhai wa Kamati ya Kutunuku ya NECTA ambayo iligeuka kuwa mahakama ya kuwahukumu watahiniwa kwa vigezo tata. Kila mwaka Kamati ya Kutunuku ya NECTA iliamua alama ya ufaulu kwa kila somo. Utaratibu huu unaruhusu Kamati ya Kutunuku kupanga shule gani iwe ya kwanza na ipi ifuatie kwa kubadili ufaulu katika somo kwa mwelekeo huo. Q3. Unadhani mabadiliko haya yanaweza kusaidia kukuza zaidi kiwango cha elimu nchini? Kupandisha kiwango cha elimu nchini ni jambo linalohitaji hatua nyingi kuchukuliwa kwa pamoja kama ilivyoainishwa katika mpango wa serikali wa matokeo makubwa sasa (BRN) katika sekta ya elimu. Na wala serikali haijasema kwamba viwango hivyo vya ufaulu vimewekwa ili kukuza ubora wa elimu nchini. Hata hivyo ni wazi kwamba viwango hivyo vitaboresha ufaulu wa wanafunzi walioandaliwa vyema na kuondoa mapungufu ya mfumo wa awali ambapo wanafunzi walipewa daraja sawa kwa ufaulu tofauti. Mfamo mwaka 2011 katika somo la Bible Knowlegde daraja B lilianza na alama 65. Lakini mwanafunzi aliyefanya mtihani wa Elimu ya Dini Ya Kiislamu alipata daraja B baada ya kupata alama 70. Utaona kwamba katika somo hili la pili alama 65, 66, 67, 68 na 69 zote zilikuwa C. Lakini kwa somo la Biblia alama hizo zote zilikuwa B. Kwa utaratibu kama huu Kamati ya Kutunuku ya NECTA inaweza kuamua kupunguza daraja la kwanza katika shule fulani kwa kubadili ufaulu bila kujali alama alizopata mtu. Mwaka 2012 majibu ya kidato cha sita yalipotangazwa alama 0-41% zilihesabiwa kwamba ni F. Alama 70 hadi 85 zilihesabiwa kuwa daraja B katika somo la advanced mathematics. Hali kama hii inawakatisha tamaa wanafunzi walioko nyuma baada ya kuona kwamba mwanafunzi waliyekuwa wakimtegemea anapata daraja la chini. Kwa kutumia mifano hiyo tangazo hilo la serikali linaweza kuboresha ufaulu na hivyo kwa watakaotumia kiwango cha ufaulu kama alama ya kuimarika ubora wa elimu basi viwango vitakuwa vimepanda. Q4. Serikali imetangaza pia alama za darasani kuwa 40 na zijumuishwe katika mtihani wa mwisho. Umeupokeaje uamuzi huo? Kwanza hili si jambo jipya. Kwa mujibu wa nyaraka za NECTA zilizokuwa mikononi mwa wateja wake alama hizo zimetajwa kuwa ni 50. Hivyo serikali imezipunguza hadi 40. Labda kwa taarifa ya wasomaji ieleweke kwamba katika mtaala unaotumika sasa ambao unataka ufundishaji ulenge kukuza umahiri (Competence Based Training) tathmini inatakiwa kuunganishwa na usomeshaji. Hivyo huko tuendako inatarajiwa kwamba alama za shule ziwe na uzito zaidi kuliko zile za mtihani wa mwisho. Na kama hili haliwi lengo la elimu ya Tanzania kumwezesha mwalimu kutoa tathmini ya kuaminika na kutegemewa basi tutakuwa tunatania. Q5 Kuna shaka kwamba huenda walimu wakapika alama hizo, unadhani hilo litawezekana? Kwa utaratibu uliotangazwa na serikali shule itatoa alama 15 tu kati ya hizo 40. Nyingine 15 zitatoka mtihani wa taifa wa kidato cha pili na 10 zilizosalia zitatoka katika mitihani ya Kanda. Kwa hiyo kama kuna Mkuu wa Shule atakayejaribu kutoa taarifa za uongo basi ni hizo alama 15. Ukweli ni kwamba kila atakayefanya hivyo ataweza kugundulika kirahisi kwa sababu kutakuwa na mpishano mkuwa kati ya alama hizo 15 na zile 25 zilizosalia na pia na zile 60 za mtihani wa mwisho. Kwa hiyo watu hao watashughulikiwa kama wahalifu. Kwa bahati mbaya wanaopinga utaratibu uliotangazwa na serikali wameshika bango kwamba kuna hatari ya walimu kughushi alama hizo, bila kuwajulisha wananchi ukweli kwamba NECTA imekuwa ikitumia alama ambazo hazijulikani kokote na hivyo kutoa mwanya wa kufelisha wanafunzi hasa wale waliojiandaa vizuri. Ndiyo sababu matokeo ya kidato cha nne mwaka 2012 yalitoa kituko cha aina yake kwani hata shule zinazofahamika kwa kufaulisha vizuri sana kama Loyola ya Dar es salaam na nyinginezo nazo zilifelisha kwa kiwango kilichowaacha wenye shule hizo wakiwa hoi. Sielewi ni kwa nini watu hawa wenye hasira na mambo ya elimu hawawezi kuhoji uhalali wa NECTA kujiamulia kuchakachua CA za wanafunzi wa nchi nzima badala ya kufuata miongozo waliyotoa wenyewe, badala yake wanaungana kuleta hoja eti walimu hawaaminiki hata kwa alama 15. Jambo hili ni kuwakosea adabu walimu wa nchi hii ambao wanaendelea kufanya kazi katika mazingira magumu na kupitia kwao hao wasiowaamini walimu wametoka na leo wanaweza kujenga hoja! Q6. Ipi njia sahihi ya kuthibiti usahihi wa alama za maendeleo zitakazokuwa zinatumwa NECTA. Kwa kweli ulinganishi wa ufaulu wa mtihani wa mwisho na alama za CA unaweza kuwa ni njia bora ya kujua ikiwa alama zilizowasilishwa zimechezewa. Inategemewa kusiwe na muachano usioelezeka wa alama hizo. Q7.Una uzoefu wa kazi ya ualimu kwa zaidi ya miaka 20, unayaonaje maendeleo ya sekta ya elimu, hasa ndani ya kipindi ambacho wewe umekuwa mwalimu? Nimeanza rasmi kazi ya ualimu mwaka 1993 na hadi sasa bado naendelea kusomesha. Yako mambo mengi makubwa yakiwemo ya kisera yaliyofanyika hadi sasa katika juhudi za serikali na watu wake za kuifanya nchi ya Tanzania iweze kushindana na wenzake katka dunia hii ya utandawazi. Utekelezaji wa mpango wa kimataifa wa elimu kwa wote (EFA) wa miaka ya 1990, utekelezaji wa malengo ya millennia yanayohusika na elimu (MDGs), upanuzi na uboreshaji wa elimu ya msingi na sekondari kupitia MMEM na MMES, kuwepo sera mpya ya elimu na mafunzo ya mwaka 1995 iliyoweka utaratibu wa ubinafsishaji na ushirikiano wa sekta binafsi na serikali katika utoaji wa elmu .Uanzishwaji wa shule za sekondari za wananchi (shule za kata). Kupanuliwa na kuimarishwa vyuo vya ufandi maarufu kama VETA, Upanuzi mkubwa wa elimu ya Juu ulioshuhudia serikali ikitoa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma vyuo vikuu ya umma na vya binafsi. Serikali inaendelea kutekeleza ugatuzi mkubwa katika sekta ya elimu unaokusudiwa kuwapa wananchi mamlaka zaidi na ushiriki mkubwa katika kutoa maamuzi ndani ya sekta ya elimu, nk. Kwa tathmini yangu kipindi hichi kimeshuhudia mapinduzi makubwa ya sekta ya elimu kuwahi kutokea katika historia ya Tanzania. Nchi inaendelea kukabiliwa na changamoto kubwa ya kuhakikisha kwamba elimu yetu inakuwa na ubora unaokubalika kimataifa.
Posted on: Tue, 03 Dec 2013 15:07:05 +0000

Trending Topics



Recently Viewed Topics




© 2015